Skip to main content

Kuhusu Viwawa

HISTORIA YA VIWAWA TANZANIA
VIWAWA ilianzishwa mwaka 1924 mji wa Brussel nchini Ubelgiji na Kadinali Joseph Cardjin nakupitishwa rasmi kama Chama cha Kitume cha Vijana Kimataifa na Baraza la Kipapa Vatcan mwaka 1950.Kadinali Joseph Cardjin pia alianzisha YCS,hivyo VIWAWA na YCS alianzisha yeye.

Makao Makuu ya Viwawa Duniani Yako Roma – Italia.
Viwawa iliingia Tanzania mwaka 1959 katika Parokia ya Msimbazi, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, chini ya Mwanzilishi Pd. Lucas Gaemperle OFM, badaye mwaka 1960 alifika nchini kwetu Pd. Hendrikus Johannes Brinkhof maarufu kama Pd Mansuetus ambaye alimsaidia kwa karibu sana, padri Lucas kuueneza utume wa viwawa nchini kwetu, na kufuatiwa na Parokia ya St. Joseph, Kurasini,Magomeni,Chang’ombe, Kibaha.

Mwanzilishi wa viwawa duniani Kardinali Joseph Cardijn alitembelea Tanzania, jimbo la Dar es salaam tarehe 17 – 6 – 1960.

Padri Lucas Gaemperle OFM ambaye alikuwa mwanzilishi wake alitembea sehemu nyingi za Afrika na Ulaya kwa lengo la kujifunza utume huu. Mwaka 1961 VIWAWA Tanzania walitembelewa na mjumbe kutoka Makao Makuu Roma Italia na alitembelea matawi ya Dar es Salaam na Moshi. Mjumbe huyo alifanyakazi ya kuunganisha utume huu hapa Tanzania na huko Zambia. Mwezi Novemba 1964 Kamati kuu ya VIWAWA ulimwenguni walifanya mkutano hapa Tanzania, Mkutano huu ulifuatiwa na ziara za mafunzo ili kuona maendeleo ya Viwawa hapa Tanzania.

Mnamo mwaka 1966 Viwawa walifanya mkutano mkuu wa kitaifa na ni majimbo mawili tu ndiyo yalihudhuria Dar es Salaam na Moshi yakiwakilishwa na wajumbe kumi na mmoja. Mwaka 1973 mkutano mkuu ulifanyika jimboni Iringa na ndipo kwa mara ya kwanza katiba ya Viwawa iliundwa, na kupitishwa rasmi kama chama cha kitume cha vijana na Baraza la Maaskofu katoliki Tanzania (TEC) mwaka 1979. Mshauri wa kwanza wa viwawa Taifa Padri Pius Shayo aliyeteuliwa katika mkutano mkuu wa baraza la maaskofu Tanzania uliofanyika tarehe 23 – 27 October, 1979.
Baada ya kupitishwa hapo kilitambulika pote Tanzania kama Chama cha Vijana Wakatoliki Wafanyakazi Tanzania (VIWAWA)Mpaka sasa, chama hiki kipo majimboni, kuanzia ngazi ya Jumuiya, Mtaa, Kanda, Kigango, Parokia, Jimbo, Taifa na Kimataifa.

MAANA YA VIWAWA
VIWAWA ni chama cha kitume cha Vijana Wakatoliki Wafanyakazi ambao wanatumwa na Kanisa ili kueneza habari njema ya kwamba Yesu Kristu ndiye njia ya ukweli na uzima kwa vijana wote katika maisha yao ya kila siku.

Wafanyakazi: Ni vijana wa wanaume na wanawake waishio mijini, vijijini na walio kwenye masomo, mafunzo ya fani mbalimbali, walio katika ajira rasmi na zisizo rasmi.

Viwawa ni chama ambacho kinawaunganisha vijana na kuwasaidia waone hali yao, kuamua juu yake katika mwanga wa Injili na kuwaongoza kufanya matendo ya kubadilisha hali zao na kutengeneza ziwe nzuri zaidi kwa njia ya Tafakari ya Maisha. Chama hiki huongozwa na vijana wenyewe katika ngazi zote na huwa na Mshauri na Mlezi kwa ngazi ya Parokia,Jimbo na Taifa.

DIRA YA VIWAWA
Kumwona Kijana Mkatoliki Mfanyakazi anayejimudu katika maisha yake ya kimwili na kiroho kwa kutumia njia ya Tafakari ya Maisha.

UTUME WA VIWAWA

Kumwezesha kijana kuwa Mkristo wa kweli ambaye ana ujasiri wa kurekibisha, kuendeleza na kudumisha taratibu za utamaduni, uchumi, siasa na utaalamu kufuatana na mpango wa Mungu.

MALENGO YA VIWAWA
Kuwawezesha Vijana kutambua wajibu wao katika kujielimisha na kujitegemea katika maisha yao.

Kustawisha na kusaidia Kanisa kwa kushiriki katika kazi za Kanisa, kuhusu maendeleo ya Kiroho, Kimwili, Kiakili na Kijamii.

Kutangaza habari za Kanisa na kujaribu kwa kila hali kuleta uhusiano mwema baina ya vyama vya kitume,madhehebu mbalimbali na dini nyingine.

Kuchukua hatua za kufaa kuendeleza mambo yote yanayoonekana kwamba ni ya manufaa kwa Kanisa na Ustawi wa jamii.

Kuwajenga vijana katika mazingira ya kuwa na mwenendo mwema kwa kanuni ya Tafakari ya Maisha inayoongozwa na mtindo wa Kuona-Kuamua na Kutenda. Na mitindo mingine ya malezi inayofaa.

Kuwakumbusha vijana wote kwamba sote tunategemeana kwa kushauriana, kuongozana na kufundishana kimwili na kiroho.

Comments